Na Haji Mtumwa, Zanzibar

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Hemed Suleiman Abdulla amesema Chama Cha Mapinduzi kimejipanga kuhakikisha Majimbo yote yanabaki kuwa chini ya CCM ifikia Uchaguzi wa Dola wa mwaka 2025.

Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ameyasema hayo wakati akizungumza na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi Jimbo la Chumbuni na Jimbo la Mpendae katika muendelezo wa ziara yake ya kuimarisha Chama.

Amesema CCM inaendelea na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025 ambapo tayari miradi mbali mbali imeshakamilika na mengine inaendelea kujengwa ambacho ni kielelezo kikubwa cha wananchi kukikubali Chama hicho hivyo, ni vyema kuendelea kuchukua jitihada ili kukiimarisha na kiweze kuendelea kushika Dola.

Hemed ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa ja Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi inaendelea kutekeleza Ilani ya CCM kwa kujenga miradi mbali mbali ambayo kukamilika kwake itazalisha ajira ambazo vijana watanufaika kwa ajili ya kujipatia kipato na kupunguza ukali wa maisha.

Aidha ameeleza kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi pamoja na wasaidizi wake wote wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanawatumika vyema wananchi wa Zanzibar kuhakikisha wanawasogezea huduma muhimu wananchi hao waliowachagua na kukikiweka madarakani Chama Cha Mapinduzi.

Pamoja na hayo Hemed ameupongeza uongozi wa Jimbo la Chumbuni kwa kuendelea kuhakikisha wanaongeza Idadi ya wanachama wa Chama Cha Mapinduzi hatua ambayo inaonesha wazi uwajibikaji wa Viongozi wa Jimbo hilo katika kuwatumikia wananchi wao.

Amewakumbusha Viongozi wa Jimbo la Chumbuni na Jimbo la Mpendae Wilaya ya Amani kichama kuhakikisha kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 ahadi zote walizoziahidi kwa wananchi wamezitekeleza ili kuwazidishia imani wana CCM na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Sufiani Khamis Ramadhan amemshukuru Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Hemed Suleiman Abdulla kwa kuamua kufanya ziara ya kuimarisha Chama kwa Majimbo yote ya Zanzibar hatua ambayo inazidisha ari na hamasa kwa wanachama wa CCM juu ya uimara wa Chama hicho.

Ameeleza kuwa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar kinaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020-2025 chini ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi kasi ambayo inadhihirisha nia thabiti na dhamira ya Dkt. Mwinyi kuwatumikia wazanzibari.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Mjini kichama Talib Ali amemshukuru na kumpongeza Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa uamuzi wake wa kutembelea majimbo yote ya uchaguzi ambapo ziara yake hiyo itawakumbusha na kutilia mkazo utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na utekelezaji wa ahadi walizoahidi kwa wananchi wakati wakiomba ridhaa.

Nae Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa Mjini Idriss Kitwana Mustafa ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi amemuahidi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kuwa Serikali ya Mkoa wa Mjini Magharibi itaendelea kusimamia Amani na Utulivu uliopo ili Serikali iweze kutekeleza vyema majukumu yake ya kusimamia Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025.

Aidha amewasisitiza wanachama wa Chama Cha Mapinduzi kuhubiri Amani na utulivu uliopo na kuepuka makundi yanayokigawa Chama.

Nao wanachama na wananchi wa majimbo hayo wamesema utekelezaji wa ahadikwa chama cha mapinduzi umepitiliza Zaidi ya makadirio hivyo, ahadi yao kwa CCM ni kuhakikisha ifikapo Uchaguzi wa 2023 kuendelea kukiweka tena madarakani Chama Cha Mapinduzi.

Please follow and like us:
Pin Share