Katia toleo liloyopita mwandishi wa makala haya alizungumzia mambo mbalimbali yanayohusu ubora, nia na malengo ya Serikali kutumia mashine za kutolea stakabadhi za malipo. Leo anazungumzia matumizi na nani anayeruhusiwa kutengeneza na kusambaza, na nani anayetakiwa  kutumia mashine hizo. Endelea…


 

Nani mtengenezaji wa mashine hizi za kielektroniki?

 

Katika mfumo huu mtengenezaji wa mashine ni yule ambaye atakuwa amethibitishwa na TRA. Wapo watengenezaji wanne wanaotambulika ambao ni Customer Engineering SPA ya Italy. RCH-SPA ya Italy, Incotex System Ltd ya Bulgaria.

Ni watu gani watahusika na uuzaji na usambazaji wa mashine?

Katika mfumo huu mpya, mashine zitasambazwa na kampuni maalum zilizopitishwa na TRA. Kwa kuanzia, wapo wasambazaji sita ambao ni Business Machine Tanzania Limited (BMTL) [email protected], Pergamon Tanzania Limited [email protected], Checknocrats Tanzania Limited [email protected], Total Fiscal Solution Limited [email protected], Compulnx Tanzania Limited [email protected], Advatech Office Supplies Limited.

Hata hivyo, majina ya wasambazaji hawa yanaweza kubadilika wakati wowote endapo watafanya kazi kinyume na makubaliano ambayo yapo kwenye mkataba.

Ni upi wajibu wa haki za wasambazaji wa mashine?

Msambazaji wa mashine atakuwa na hali na wajibu ufuatao: Kuuza, kuwafungia na kuwafundisha matumizi sahihi ya mashine wafanyabiashara wanaotakiwa kuwa na mashine hizo, kutengeneza mashine ndani ya saa 48 pale inapokuwa imeharibika.

 

Pia kutoa taarifa ya matumizi mabaya ya mashine hizo kwa mamlaka ya mapato, kutoa taarifa ya mauzo ya mashine hizo kwa mamlaka ya mapato,

Risiti zinazotolewa na mashine maalum za kielektroniki zikoje?

Risiti zitakazotolewa na mashine zina muonekano ufuatao; risiti itaanza na maneno “Risisti halali” na kumalizikia na

“Risiti halali”, Jina na anuani ya mtumiaji wa mashine.

 

Namba ya uandikishaji wa VAT (VAT Registration Number-VRN) Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN), ya mtumiaji wa mashine, jina na anuani ya mnunuaji, Namba ya Utambulisho wa Mashine (EFD licence number).

Pia inaonesha Jina, kiasi, bei, maelezo, kiwango cha kodi kwenye bidhaa au huduma iliyotolewa, kodi halisi, punguzo la bei, mabadiliko na masahihisho yoyote katika bidhaa au huduma, tarehe na muda wa kutoa risiti, jumla kuu ya kodi, mfuatano kamili wa risiti zinazotolewa, nembo ya TRA.

Ankara za mashine za kielektroniki za kodi zitakuwa na sura gani?

Mashine zitakuwa na sura zifuatazo; Ankara ya kielektroniki, jina na anuani ya mtumiaji wa mashine, Namba ya Utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN) na Namba ya Usajili wa VAT (VRN), Jina na anauni ya mnunuaji wa bidhaa/huduma mwenye TIN na VRN, Namba ya utambulisho wa mtumiaji wa mahine, alama ya mashine, jina, kiasi, bei, maelezo, kiwango cha kodi kwenye bidhaa au huduma iliyotolewa, jumla kuu.

Punguzo la bei, mabadiliko na masahihisho yoyote katika bidhaa au huduma, mfuatano kamili wa risiti zinazotolewa, Nini tafsiri ya “Z” rpoti?

“Z” ripoti ni muhtasari wa mauzo yote yaliyouzwa kupitia mashine za kielektroniki za kodi, kwa siku, mwezi au kwa mwaka, ripoti hiyo inasaidia kutambua kwamba mauzo yote yamelipiwa kodi, na uhakika wa kutosha upo kuonesha kwamba kodi haikupotea.

 

“Z” ripoti ina sura gani?

“Z” ripoti ina sura zifuatazo; Itaanza na maneno “Risiti halali” na kumalizikia na “Risiti halali”.

Jina au jina la biashara na anuani yake, Namba ya usajili wa VAT, Bidhaa/huduma zinazotozwa kodi, Namba ya utambulisho wa mlipa kodi (TIN) nay a usajili wa VAT (VRN).

Ofisi ya kodi iliyoidhinisha mashine, Ripoti lazima ianze na “Z” ikimaanisha mauzo ya siku, Ripoti “Z” ya kila siku iwe katika mfuatano; Namba ya utambulisho wa kila mashine endapo zimetumika zaidi ya moja katika biashara, muda na tarehe “Z” ripoti ilipotolewa.

 

Mauzo ya siku na jumla ya mauzo yote yaliyofanyika, ripoti tokea tarehe mashine iliposajiliwa, namba ya utambulisho wa uidhinishaji wa rejesta ya kodi.

Upunguzaji wa gharama kwenye kodi (cost offset) ina maana gani?

Serikali imeamua kufidia gharama za ununuaji wa mashine za kwanza za kielektroniki za kodi kutoka kwa wafanyabiashara waliosajiliwa na Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).

Lengo ikiwa ni kupunguza gharama za ununuaji wa mashine za kielektroniki za kodi na hivyo kujenga uhiari wa kulipa kodi.

Utaratibu wa kujipunguzia gharama hizi ukoje?

Serikali imetambua umuhimu wa mashine hizi hivyo imeamua kutoa unafuu wa ununuzi na watumiaji hawataingia gharama ya moja kwa moja katika ununuzi. Gharama watakazoingia katika ununuzi wa mashine zitakazonunuliwa kwa mara ya kwanza watarudishiwa.

Gharama hizi zitarudishwa kwa watumiaji hao kwa njia ya kupunguza kwenye marejesho ya ritani ya VAT yaani Input Tax”.

Gharama hizi zitahusu bei ya mashine pekee na haitahusisha usafirishaji, kwenda kwa mtumiaji (transportation), ufungaji wa mashine (installation) n.k

 

Endapo kwa mwezi husika gharama ile haikuweza kupunguzwa yote itaendelea kufidiwa katika mwezi mwingine mpaka itakapokwisha.

 

Na endapo itafika miezi sita gharama hii haijaisha kufidiwa basi utaratibu wa kawaida wa madai ya marejesho utafuatwa.

Utaratibu ukoje endapo mashine haifanyi kazi?

Endapo itatokea kwamba mashine imeshindwa kufanya kazi, mtumiaji wa mashine atatakiwa kutoa taarifa kwa msambazaji na Ofisi ya TRA ndani ya saa 24.

Msambazaji vilevile amepewa jukumu la kufanya marekebisho hayo ndani ya saa 48. Matengenezo mengine ya kawaida ya mashine yatafanywa kadiri ya muda na makubaliano yatakavyofikiwa baina ya mtumiaji na msambazaji.

Kwa vile mashine itakuwa haifanyi kazi na biashara inatakiwa iendelee, mtumiaji wa mashine ameruhusiwa kutoa risiti kwa kutumia vitabu vya mauzo.

Mashine ikitengemaa sheria inamtaka ayaingize kwenye mashine mauzo yote aliyoyatoa kwa kutumia risiti ambazo hazitolewi na mashine.

Mtumiaji wa mashine asipotumia mashine katika mauzo ni kosa?

Ndiyo. Sheria inamtaka kila mtumiaji wa mashine kuzitumia kila anapofanya mauzo katika biashara. Mtumiaji yeyote ambaye atauza bila kutumia mashine ni kosa na ataadhibiwa kulingana na sheria.


 

By Jamhuri